Monday, March 10, 2014

MARIA IMAKULATA

Mafundisho ya Kanisa kuhusu Mama Maria kamwe si mageni bali yalisimamiwa na Kanisa na wakristu wote toka karne ya kwanza baada ya Kristu. Itakua ni vyema kutoa kwa ufupi historia ya fundisho hilo linalomhusu Mama Maria. Kanisa linafundisha kuwa katika kipindi chote cha maisha yake duniani, Mama Maria kwa neema za Mungu hakutenda dhambi wala hakua na doa la dhambi. Kanisa hilo Moja la mitume la Mashariki (Orthodox) na Magharibi (Roma Katoliki) hata baada ya kuvunjika umoja wao mnamo mwaka 1054 karne ya 11, bado linafundisha na kushikilia imani hiyo mpake sasa. Kwa huzuni kubwa Kanisa la magharibi (Roma Katoliki) pia likavunjika karne ya 16 na kutengeneza pande mbili za Waprotestanti na Wakatoliki huku baadhi ya Waprotestanti wakikataa fundisho hilo japo si wote kama ilivyobaki kwa Martin Luther ambaye hakuonyesha kupinga. Heshima aliyokuwa akipewa Mama ikapuuziwa na msaada wake wa kutuombea na kuturudisha kwa mwanaye Kristu ukakataliwa na baadhi ya wakristu. Hivyo basi Kanisa la magharibi likaendelea kugawanyika katika mafundisho yake. Ili wakatoliki wasitetereke katika imani yao juu ya Mama Maria, mnamo mwaka 1854 Baba Mtakatifu Pius IX (Mwenye Heri) kama mrithi wa kiti cha Mtume Petro, kupitia mamlaka aliyopewa ya kufunga na kufungua (Mathayo 16:19) akatangaza kupitia heshima ya kiti hicho yaani ex cathedra fundisho la imani yaani Dogma ambalo humpasa kila mkatoliki kuamini bila kupinga kwa kuwa dogma ni fundisho la Roho Mtakatifu mwenyewe. Hivyo kama Dogma, Mama Maria akatangazwa kuzaliwa bila dhambi ya asili yaani Immaculate Conception. Neno Imakulata (immaculate) maana yake ni usafi usio na doa la uchafu.

Iliwezekana vipi Mama Maria kukingiwa dhambi ya asili na kuishi bila dhambi?

Injili ya Luka inatuambia kuwa malaika Gabrieli anamsalimu Mama Maria kwa salamu ya pekee kabisa akisema "Salamu Maria umejaa Neema, Bwana yu nawe" (luka 1:28). Neema basi ni kitu gani? Neema ni zawadi ya bure itokayo kwa Mungu Baba, zawadi hii kwa mafundisho ya Mtume Paulo ndiyo ituokoayo (Waefeso 2). Hakuna binadamu kwa matendo yake mwenyewe anaweza kuokolewa bila Neema ya Mungu. Tukiendelea kutafakari salamu ya malaika Gabriel, tunakutana na neno "umejaa neema". Neno kujaa linaashiria kipimo kamili kabisa kisichokua na upungufu hata kidogo. Hivyo Mama Maria alijazwa Neema ya pekee kuliko ya mtu yeyote yule. Neema hiyo ndiyo iliyomfanya aweze kushinda majaribu yake yote. Lakini Je, jambo hili ameweza kulifanya kwa nguvu zake mwenyewe. HAPANA, Mama Maria alifahamu kwamba naye aliokolewa kwa kukingiwa dhambi hivyo anasema katika mwimbo wake "Magnificat " akisema “Na roho yangu inamfurahia Mungu Mwokozi wangu” (Luka 1:47). Neema itokayo kwa Bwana ndio iokoayo. Mama Maria ni binadamu na ni kiumbe cha Mungu kama sisi wote tulivyo. Lakini kwa ule utayari wake katika kushiriki ule mpango wa Mungu wa kuikomboa Dunia kwa kukubali kwa hiari na kusema NDIYO (..Na iwe kwangu kama ulivyosema (Luka 1:38) na kwa neema tele za Kristu mwanaye, basi Mungu toka milele alimpatia Maria neema hiyo kabla hata hajamuumba. Ndipo wanakoliki tunapokiri kwamba Mama alikingiwa dhambi ya asili kabla hata ya kuumbwa yaani Immaculate Conception. Japo Maria ni binadamu kamili kama sisi, tofauti ni kuwa sisi tunazaliwa na dhambi hiyo na tunahitaji neema ya Sacramenti ya Ubatizo ili tufutiwe dhambi hiyo. Ndio maana Kristu alitoa amri kwa wafuasi wake watangaze injili na kubatiza watu wote katika kanuni ya Utatu Mtakatifu (Mathayo 28:19). Japo Mama alipewa neema kamili, kamwe hakuondolewa uhuru wa nafsi yake anayopewa kila binadamu ya kuchagua jema ama baya yaani free will. Wanaopinga fundisho hili la imani wakumbuke kuwa Mungu ni muweza wa yote, aliumba kila kitu na kuona ni chema (Mwanzo 1:31) Hivyo Adam na ubavu wake (Eva) waliumbwa wema bila doa la dhambi. Dhambi ilikua haijaingia duniani, hivo kama ilivo kwa Maria, Adam aliumbwa safi (Immaculate). Iweje tena Mungu ashindwe mfanyia mwanamke aliyebarikiwa kuliko wanawake wote? (luka 1:42) Kuliko hata Eva, ambaye naye aliumbwa bila dhambi ya asili? Lakini hata hivo Mungu hakumuondolea Adam zawadi yake ya nafsi kuwa huru katika kuchagua. Adam kupitia Eva akachagua baya na dhambi ikaingia duniani kwa kupitia kwake. Hivyo kila mzaliwa wa Adam anarithi dhambi hiyo ya asili na kwa ajili ya dhambi moja kifo kikaingia duniani (Warumi 5:12).  Ndio maana Kristu akamwambia Nikodemu Kweli nakwambia, mtu asipozaliwa kwa maji na Roho, hawezi kamwe kuingia katika ufalme wa Mungu”(Yohana 3:5)




Je, kama Mama Maria amekingiwa dhambi ya asili toka milele, wapi tunapata habari hizo katika Biblia?

Turejee kitabu cha Mwanzo ambapo Mungu anamwelezea mwovu shetani jinsi atakavyo ikomboa dunia. Anasema nitafanya Uadui kati yako na mwanamke, mbegu yake itakanyaga kichwa chako (Mwanzo 3:15). Katika kutafsiri mstari huu, Kanisa na Mababa wa Kanisa wanatafakari, Je, mbegu hiyo ni ipi (Nani) atakaye mkanyaga shetani?  Wakristu wote tunaafiki na kukiri pamoja na Kanisa kuwa mbegu hiyo (huyo) ni Kristu mbarikiwa. Kwa kifo na ufufuko wake ameshinda mauti na kumkanyaga shetani. Hivyo yeye ndiye mbegu. Na kamwe Kristu kwa kuwa hakuwa na dhambi hata kidogo (1 Yohana 3:5) hawezi kutoka kwenye mbegu yenye dhambi. Bali yampasa kutoka kwenye mbegu safi. Hivyo huyo mwanamke Mungu aliyemtaja ni Mama Maria na si Eva. Kwani mbegu ya Eva na Adam ni sisi binadamu wote na kwa dhambi ya mtu mmoja (Adam) kifo kikaingia kwetu wote. Lakini Mababa wa Kanisa wakaendelea kutafakari neno "Nitafanya uadui….". Mungu kwa Neema yake anatengeneza “Uadui " kati ya Maria na Shetani. Jambo hili limefanyika miaka karne nyingi kabla hata ya kuzaliwa Maria. Neno uadui ni kukosa mapatanisho na kutoelewana. Tunatengeneza uadui na Mungu pale tunapo tenda dhambi. Pia tunatengeneza uadui na shetani pale tunapotenda mema. Hivyo kwa Mungu kutengeneza uadui kati ya mwanamke (Maria) na shetani, anampatia Maria neema yake ya pekee ili daima Maria atende mema na milele awe adui wa shetani kwa kukataa kutenda dhambi hata zile ndogo. Kama Maria katika maisha yake duniani angeweza hata mara moja kuwa rafiki wa shetani kwa kutenda hata dhambi ndogo tu,  Je,  tuseme basi Mungu ameshindwa tekeleza ahadi yake juu ya mwanamke huyu? HAIWEZEKANI, kwani imeandikwa Mungu ni muweza wa yote (Mathayo 19:26, Luka 1:37, Marko 10:27 ), pia imeandikwa Bwana hakawii kutimiza ahadi yake (2 Petro 3:9), na  pengine tunakiri Mungu si binadamu kubadilisha mawazo yake (1 Samueli 15:29 )

Tunaelewaje kuhusu Utakaso wa Maria katika Hekalu la Bwana(Luka 2:22), Je mstari huu haupingani na fundisho hili?

“Siku zilipotimia za Yosefu na Maria kutakaswa kama walivyotakiwa na Sheria ya Musa, wazazi hao walimchukua mtoto, wakaenda naye Yerusalemu ili wamweke mbele ya Bwana”

Mstari huu unazungumzia Maria aliyehitaji kutakaswa Hekaluni baada ya kumzaa mtoto Yesu. Hii ilikua ni sheria ya Torati ya Musa iliyohitaji kila mwanamke baada ya kujifungua, inampasa kujitokeza mbele ya Hekalu la Bwana na kutoa sadaka ili apate kusafishwa dhambi ya uchafu uliotokana na kujifungua. Kama Maria alikua msafi asiye na doa la dhambi mbona ilimpasa pia yeye kusafishwa? Hapa jibu linalotolewa ni sawa na jibu alilotoa Kristu kwa Yohana Mbatizaji wakati Yesu anakuja kubatizwa naye. Ubatizo wa Yohana ulikua ni wa Toba na wa kuondolewa dhambi na kusafishwa. Lakini Yesu asiye na doa la dhambi hakuhitaji ubatizo huo. Pia hakuja kutengua sheria ya Torati, hivyo ili haki itendeke anamwambia Yohana “Acha tu iwe hivyo kwa sasa, maana kwa namna hii inafaa tuyatekeleze yale yote Mungu anayotaka” (Mathayo 3:15). Ni hivyo hivyo ilivyotendeka kwa Maria alipohitaji kusafishwa kutokana na sheria za Torati. Si kusafishwa kwa ajili ya dhambi maana hakua na hata moja. Bali alikubali na kuheshimu sheria ili “haki yote itendeke”

Maria Sanduku Jipya la Agano

Katika kitabu cha agano la kale, kama jinsi Mungu alivopendelea kukaa ndani ya Sanduku la Agano ambalo lilikua takatifu na lenye usafi, vivyo hivyo alipendelea kushuka duniani na kukaa miezi tisa ndani mwa sanduku jipya la agano lililo safi yaani Mama Maria. Hivyo basi ndio maana Kanisa hadi hivi leo kupitia mafundisho ya mababa wa Kanisa na mapokeo ya mitume, Mama Maria anaitwa Sanduku jipya la Agano maana Mungu alikaa tumboni mwake kwa miezi tisa. Mt Luka katika injili yake anatupatia uhusiano huo kwa kuonyesha furaha aliyopata Yohana mbatizaji akiwa tumboni mwa mamaye Elizabeth wakati Maria amekwenda mtembelea. Elizabeth anasema mtoto Yahona alicheza kwa furaha. Vivyo hivo Mfalme Daudi pia alicheza kwa furaha mara tu baada ya kurudishwa Sanduku la agano ambapo ndani yupo Mungu (2 Samueli 6:14)). Elizabeth bila hata kujua habari alizopashwa Maria, anajazwa na Roho Mtakatifu na kumlaki Maria kama Mama wa Bwana ambaye ni Mungu mwenyewe katika nafsi ya pili

Mwisho kabisa Mama Maria mwenyewe amedhihirisha ukweli wa fundisho hili kwetu. Kila mwaka ifikapo tarehe 11 Februari, Kanisa huadhimisha sikukuu ya Mama yetu wa Lourdes ambapo tunakumbuka Mama Maria kumtokea Mt Benardetta na kujitambulisha jina kama "Ni mimi niliye kingiwa dhambi ya asili " peleka ujumbe wangu kwa wote kwamba watubu na kusali na kumwamini Yesu Kristu ili waokoke. Maria alimtokea kwa mara ya kwanza Mt. Benardeta mwaka 1858 huko Loudes ufaransa

Je, aheshimike Milele?

Anayekubali mafundisho haya ndiye mshika neno la Mungu katika uhalisia wake. Neno la Mungu linatusihi kumheshimu Mama daima katika vizazi vyote vya kale na vijavyo. Biblia inatuambia kuwa tangu kutungwa mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, inatupasa watu wote kumwita Mama Maria “Mwenye Heri”. Hivyo tangu sasa watu wote wataniita mwenye heri (Luka 1:48). Biblia kutumia neno “Tangu sasa” inataka kutuonyesha kuwa heshima anayopata Mama Maria hadi hivi leo si ngeni kama ilivyoanza kukataliwa na wakristu wenzetu karne ya 16. Heshima hiyo alipewa “Tangu” kipindi kile cha Kristu. Biblia ya Kiingereza inatumia maneno “All generations will call me blessed”. Maneno “All generations” ikimaanisha kila kizazi cha binadamu toka kipindi cha Kristu, kipindi cha matendo ya Mitume, kipindi tunachoishi kwa sasa na daima kitamheshimu Mama wa Mungu na kumwomba atuombee kwa mwanaye Kristu Mfalme ili tupate wokovu

Maria Mama wa Mungu, utuombee sasa na wakati wa kufa kwetu. AMINA 

Monday, March 3, 2014

MAPOKEO YA MITUME NA BIBLIA

Kristu akitabiri ujio wa Roho Mtakatifu, aliwaambia Mitume wake, Ninayo bado mengi ya kuwaambieni, ila kwa sasa hamwezi kuyastahimili, Lakini atakapokuja huyo Roho wa kweli atawaongoza kwenye ukweli wote….. atawaambieni yale atakayopata kutoka kwangu (Yoh 16:12-14)

Hivyo katika siku ya Pentecost wakiwa Mitume wako pamoja na Mama Maria na wanawake wengine (Matendo ya Mitume 1:14), Roho Mtakatifu akawashukia na ndio rasmi Kanisa likazaliwa na Roho Mtakatifu akakaa nao milele. (Matendo ya Mitume 2:1-4). Mitume wakapewa jukumu la kufundisha na kusimamia ukweli

Je, ukweli huo umetufikia kwa njia ya maandishi tu yaani Biblia Takatifu peke yake?


Ni lazima kusisitiza kabisa kwamba Biblia ni Neno la Mungu na Mungu ndiye mwandishi wakes. Pia kama Neno, ndani mwake hamna upotovu hata kidogo. Wakatoliki wote inatupasa kuamini na kukubali yote yaliyoandikwa katika Biblia kama ufunuo kutoka kwa Mungu. Lakini wakatoliki tunaamini kuwa Si Biblia peke yake yenye chanzo cha ufunuo wote kamili aliokusudia Kristu. Linaonekana ni jambo la kushangaza sana lakini Biblia yenyewe inakubaliana na huu ukweli kwamba si kila kitu alichotenda na kuagiza Kristu kimeandikwa na karamu yaani kwa njia ya maandishi (Yohana 21:25)

Ni kwa njia gani nyingine basi ufunuo wa Kristu umetufikia?

Historia inaonyesha kwamba Mitume, kama ilivyokuwa kipindi cha Kristu walieneza Injili kwa kuhubiri kwanza kabla ya kuweka Imani katika maandishi. Wote 12 na wale wafuasi 70 walipewa jukumu la kusambaza habari njema. Lakini Biblia yetu inavyo vitabu 27 tu vya agano jipya na kati ya hivyo 12 vimeandikwa na Paulo peke yake. Je, kazi za Mitume wengine zilizokosekana basi zimekosa ukweli? Historia ya Kanisa huzungumzia kuwa katika kitabu cha Agano Jipya, kabla hata ya Injili (Mathayo, Marko, Luka na Yohana) nne kuandikwa, waraka wa kwanza kuandikwa ulikua ni barua ya kwanza ya Paulo kwa Wakorintho. Baadaye ndio ikaandikwa Injili ya kwanza ya Marko aliyekua mwanafunzi wa Mtume Petro. Kama mwanafunzi wa Petro, Marko hakushuhudia kwa macho uwepo wa Yesu duniani bali alipewa ufunuo huo na Petro mwenyewe kwa njia ya mafundisho na si kwa maandishi. Ndipo basi ikaandikwa Injili ya Marko ambayo ni ya kwanza kabisa katika Injili nne. Japo katika list ya Injili imewekwa namba 2 katika Biblia. Baada ya Marko ndipo zikaandikwa Injili nyingine za Matayo, luka na mwisho Yohana. Pia zikafuata nyaraka mbali mbali za mitume kama tunavyozishuhudia katika agano jipya. Ifamike kwa undani kabisa kwamba zilikuwako Injili nyingi mno zaidi ya hizo nne, pia ziliandikwa nyaraka mbali mbali nyingi zaidi ya zile tunazofahamu kwenye Biblia. Yasemekama kwa jumla kulikua na nyaraka na vitabu zaidi ya 80. Kumbe Agano jipya lenye vitabu 27 tu vya ukweli vilichaguliwa katika ya vingi sana vilivyokuwa vimeandikwa lakini vya kupotosha Imani. Hapo ndipo unapatikana umuhimu wa kutenganisha neno la Mungu na maandishi ya vitabu. Kanisa liliamua neno la Mungu linapatikana katika vitabu 27 tu vya agano jipya pamoja na vile vya agano la kale. Ni Kanisa (Katoliki la Mitume) lililo amnua juu ya Idadi ya vitabu vya Biblia kwa mara ya kwanza mnamo Karne ya nne mwaka 393 katika mtaguso wa Hippo. Idadi hiyo ya vitabu ndiyo itumikayo mpaka sasa. Twaweza jiuliza, Je, Biblia tuliyonayo ndiyo yenyewe iliyomua idadi ya vitabu? HAPANA, maana kama kitabu kamili na mkusanyiko wa Injili na Nyaraka bado hakikuweko. Je, paliwahi kutokea Malaika aliyetumwa kutoa Idadi ya vitabu?  HAPANA, Je ilikua ni kazi ya Roho Mtakatifu kupitia Kanisa Katoliki na mababa wa Kanisa? NDIYO. Lakini hili liliwezekana vipi?  Ndicho tunachojaribu kuelezea hapa

 Historia inaonyesha kuwa kulitokea machafuko makubwa nchini Israel mwaka 70 baada ya Kristu. Hizi zilikua ni jitihada za wayahudi kuleta mapinduzi juu ya utawala wa Roma nchini mwao.Machafuko haya yalitabiriwa na Kristu katika Injiliya Matayo alipozungumizia kuanguka kwa Hekalu na kutoa amri kwa wafuasi wake yaani wakristu kukimbia mara tu machafuko haya yatakapo anza kutokea (Matayo 24:15-21)


Hivyo Kanisa na wakristu Israeli wakasambaratika na kuzidiwa nguvu. Wakristu wengi walikimbia nchi. Kwa upande mwingine Kanisa la Roma lililoanzishwa na Mitume Petro na Paulo (ambao pia wote walikufa mjini Roma), japo dogo na changa likasimama kama Kanisa Mama na Askofu wake kupewa nafasi ya kwanza kiheshima na mamlaka ya kuhakikisha umoja katika makanisa. Kanisa hili la Roma lilijengwa juu ya miamba Petro na Paulo na ile imani ya kitume ikasimama imara. Ikumbukwe pia kuwa si Kanisa la Roma tu lililo simama katika imani ya mitume yaani Apostolic, bali kuna Kanisa la Mashariki Constantinopo wakristu wa Orthodox. Hili lilianzishwa na Askofu wake Mtume Andrea kaka yake Mtume Petro. Pia kanisa la Kitume la Alexandria Misri wakristu Oriento orthodox. Hili lilianzishwa na Askofu Marko (mwandishi wa Injili) pia na mwanafunzi wa Petro. Pia kanisa la mashariki Syria wakristu Nestorian. Pia Kanisa la kitume la India lililoanzishwa na Mtume Tomaso. Pamoja na Kanisa la Orthodox Ethiopia lililosimamiwa na Kanisa la Oriento Misri. Makanisa haya hadi hivi leo yapo na yanayo mapokeo kamili ya mitume. Lakini lenye heshima kuu ni kanisa la Roma lililoanzishwa juu ya miamba Petro na Paulo. Ni kwa kupitia imani ya mapokeo ndiyo Kanisa likaweza kuamua juu ya idadi ya vitabu vya Biblia. Hivyo imani hiyo ya mapokeo yaani Tradition ndiyo iliyotumika kuhakiki na kuchagua vitabu. Bila imani hiyo mpaka hivi leo wakristu tungebaki na changamoto ya kujua ni vitabu vipi vya ukweli na vipi ni vya kupotosha.

Je, Mapokeo ya Mitume ni nini (Tradition)
Katika kueneza Injili basi mitume wa Yesu walihubiri kwa maneno na barua huku wakiongozwa na Roho Mtakatifu. Ni hapo basi ndipo tunapokutana na neno la Mungu lililohubiriwa (Tradition) lakini halikuwekwa katika maandishi (written scripture yaani Biblia)
Hili neno la Mungu la mahubiri tu ndilo tuitalo Mapokeo ya Mitume. Katika kuhakikisha imani ya mapokeo inasambazwa na kulindwa, Mitume hao 12 walianzisha makanisa mbali mbali na kuchagua viongozi yaani Maaskofu kwa kwa njia ya kuwawekea mikono wafuasi wao (1 Timoteo 4:14) na kuwafanya maaskofu. Ilipohitajika walikuza na kuimarisha imani ya viongozi hao kwa  kuwaandikia barua na nyaraka mbali mbali ambazo ndizo zimekusanywa na Kanisa na kufanywa Biblia. Kanisa lililo jengwa juu ya mwamba Petro (Matayo 16:18) ndilo liliachiwa mamlaka ya kulinda na kutafsiri Injili ya Bwana kwa maana Kanisa ni nguzo na msingi wa kweli(1 Timotheo 3:15). Kweli tuliyoipokea kwa njia hizo mbili zilizo sawa katika mamlaka kwa maana zote ni neno kutoka kwa Bwana. Kanisa hilo la mitume japo ni moja (Catholic) lakini limegawanyika katika makanisa mengi mengi lakini yenye imani sawa ya Mitume (Roma, Orthodox, Oriental orthodox, Nestorian) mpaka hivi leo linafundisha na kushikilia imani hiyo ya mitume mapokeo (Tradition) na Biblia. Ichukuliwe tahadhari kubwa ya kushawishika kutafsiri neno “Tradition” kama “tradition” yaani tamaduni. Makanisa haya yanaposema Tradition hutumia herufi kubwa “T” kukwepa tafsiri ya herufi ndogo “t” inayomaanisha tamaduni na desturi za binadamu zinazobadilika. Maana halisi ya neon Tradition ni “Mapokeo” na si ya binadamu bali ya Mitume katika ufunuo wa Roho Mtakatifu. Imani hii kamwe haibadiriki. Kwa sikitiko kubwa sana fundisho hili la mapokeo lilipingwa na kukataliwa kwa mara ya kwanza kabisa mnamo karne ya 15 na wakristu wenzetu wa Protestanti. Hii ikasababisha mgawanyiko mkubwa sana wa Kanisa hadi hivi leo huku waprotestanti wakiamini kuwa ni Biblia peke yake tu ndiyo chanzo cha ufunuo kamili. Je, Biblia yenyewe imefundisha mtazamo huu? HAPANA.. kama tulivyoona hapo mwanzo, Biblia yenyewe inakiri kuwa si yote aliyotenda na kusema Yesu yameandikwa katika Biblia (Yohana 21:25). Mengine hayapo. Pia Mt Paulo katika waraka wake kwa Wathesalonike anatenganisha nia hizi mbili na kuwasihi kwamba “….ndugu wapendwa, simameni imara na mshike sana yale mafundisho tuliyowapeni katika mahubiri yetu na kwa barua zetu (2 Wathesalonike 2:15)”. Pia katika matendo ya mitume Mt. Paulo anatamka maneno ya Yesu ambayo hayapatikani kabisa katika Injili za Biblia akiwaambia wazee wa Kanisa la Efeso akiwasihi kwamba Yesu alisema “ Kuna Baraka kubwa zaidi katika kutoa kuliko kupokea (Matendo ya Mitume 20:35). Kama maneno haya hayapatikani katika Injili basi ni dhahiri kabisa Paulo aliyapata katika Mapokeo yaliyoletwa na Roho Mtakatifu. Mfano mwingine ni katika waraka wa Mt. Yuda akiongelea ushindani kati ya Malaika Mikaeli na shetani juu ya mwili wa Musa (Yuda 1:9). Tukio hili ambalo halikuandikwa mahala popote katika agano la kale lakini Yuda alililipata kwa njia ya mapokeo. Inapatikana mifano mingi tu ya kulinda hoja hii ya ukweli katika Biblia.

Ifuatayo ni mifano ya mapokeo ya Kanisa Katoliki la Mitume ambayo haijawekwa kinagaubaga katika biblia. Ni vyema kuuliza, Je Biblia imekataza mapokeao haya? HAPANA, bali Biblia inayo mifano mingi inayotetea mapokeo haya kama tutakavyoona hapo baadaye tutakapo tembelea na kuelezea kwa undani kila moja ya mapokeo haya. Yafuatayo ni mapokeo 

1. Mafundisho yote ya Kanisa kuhusu Mama Maria
1.1  Alizaliwa bila dhambi ya asili hivyo hakua na doa la dhambi (Immaculate Conception)
1.2  Baada ya kumzaa Kristu alibaki Bikira milele (Perpetual Virginity)
1.3  Baada kumaliza mda wake alipalizwa mbinnguni mwili na roho (Bodily Assumption)
1.4  Anatuombea sisi wakosefu
2. Utatu Mtakatifu (Trinity)
3. Kuombea roho za marehemu (Pray for the dead and communion of Saints)
4. Toharani (Purgatory)
5. Kuwaheshimu Watakatifu, Malaika na kuomba maombezi yao (Veneration and Intercession of Saints)
6. Kuheshimu Mabaki ya Watakatifu (Veneration of Relics)
7. Kuheshimu (kamwe c kuabudu) picha na sanamu (Holy Icon & Statue veneration)
8. Ubatizo wa watoto wachanga (Infant Baptism)
9. Mtazamo wa Misa kama Sadaka ya Kristu (Mass as a Sacrifice)
10. Mitaguso ya kiukumeni (Ecumenical Councils)

Tutapata muda wa kuangalia kwa undani mafundisho haya moja baada ya nyingine

Wednesday, February 13, 2013

KWARESIMA

“Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuomboleza. Rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie  Bwana…” (Yoe 2:12)

Leo Kanisa limeanza kipindi cha Kwaresima. Hizi ni siku arobaini za sala, mafungo, kujinyima, kutubu na kuwasaidia wahitaji. Ni kipindi cha maandalizi ya sikukuu ya Ufufuko wa Yesu. Neno linalotuongoza ni wongofu. Kwaresima ni safari inayomrudisha mkristo kwenye njia ya wongofu: nirudieni mimi! Hivyo ndivyo Bwana anavyotuhimiza. Anataka tumrudie, si kwa matendo ya nje, bali kwa mioyo yetu yote kwa kurarua mioyo na si mavazi.


Mafungo ya Kwaresima si ya kujikatalia kula tu, bali pia kuacha kabisa mawazo, maneno na matendo yanayopunguza mwendo wetu wa safari ya kiroho. Ni kipindi cha ibada ya moyo na cha kutenda matendo ya huruma yanayoonesha mshikamano wa kibinadamu na upendo wa kikristo unaookoa. Kama anavyosema Mt. Petro Krisologo; “Matendo ya huruma na ibada ndiyo mabawa ya mfungo… mfungo bila matendo ya huruma ni sanamu ya njaa, ni muonekano wa nje usio na thamani ya utakatifu. Bila ibada mfungo ni fursa ya ubinafsi… tunapofunga, ndugu zangu, tuweke chakula chetu mikononi mwa maskini” (Petro Krisologo, Omelia VIII, Sul digiuno della Quinquagesima)

Kipindi hiki kinapaswa kuwa kipindi kinachotusaidia kuanza tukio la kinabii, tukio linalosaidia kuyabadili maisha yetu na ya wenzetu. Katika Biblia Musa anafunga siku arobaini usiku na mchana kabla ya kupokea Amri Kumi za Mungu (Rej. Kut 34:28), anafanya hivyo pia Elia kabla hajakutana na Mungu juu yam lima Horebu (1Fal 19:8), hali kadhalika Yesu kabla hajaanza utume wake.

Majivu na maji


Kipindi cha Kwaresima kinaanza siku ya Jumatano ya Majivu. Don Tonino Bello, aliyekuwa Askofu wa Molfetta, Italia anaandika kuwa safari yote ya mkristo ni kuanzia kichwani hadi miguuni. Ni safari inayoelezwa vizuri kwa ishara ya majivu tunayopakwa kichwani na maji anayotumia Yesu kuwaosha mitume wake miguu. Ni safari inayoanzia kwenye toba na kuishia kwenye utumishi. “Toba na utumishi”, anasema Don Tonino Bello, “ni mahubiri makuu ambayo kanisa linayakabidhi kwa majivu na maji, kuliko kwa maneno”. Kwa maneno mengine ndiyo kusema kuwa mahubiri yetu hayawezi kuielezea vizuri zaidi safari ya uongofu kama jinsi ambavyo ishara ya majivu na maji inavyoweza kufanya. Tumrudie Mungu kwa moyo wa toba na katika utumishi tuzidi kuiona ile sura ya Mungu katika mahujaji wote walio katika safari ya maisha. 



Tuesday, February 12, 2013

BENEDIKTO XVI ATANGAZA KUACHILIA MADARAKA YA KULIONGOZA KANISA

Baba Mtakatifu Benedikto XVI ametangaza azma yake ya kuachilia madaraka ya kuliongoza Kanisa Katoliki ifikapo tarehe 28 Februari 2013. Habari hii imepokelewa kwa hisia tofauti na kwa mshtuko mkubwa. Kulingana na taratibu za Kanisa, Baba Mtakatifu anaweza kuachilia madaraka. Sheria ya Kanisa No. 332#2 inaeleza kuwa masharti mawili ya Baba Mtakatifu kuachilia madaraka ya kuliongoza Kanisa, kwanza, ni kufikia uamuzi huo yeye mwenyewe kwa uhuru na kwa hiari yake. 


Pili, ataamke waziwazi juu ya uamuzi wake wa kuachilia madaraka. Baba Mtakatifu anaweza kuachilia madaraka pale anapopoteza uwezo wa kuongoza au inapotokea afya yake ikatetereka na hivi kushindwa kutimiza majukumu yake kikamilifu. Sababu iliyopelekea Baba Mtakatifu Benedikto XVI, ambaye tarehe 16 Aprili atatimiza miaka 85, kuachilia madaraka, kama alivyoeleza mwenyewe ni kutokana na kutetereka kwa afya yake. Akitangaza hatua yake ya kuachilia madaraka aliyoisoma kwa lugha ya kilatini, Baba Mtakatifu Benedikto XVI alisema:


“Ndugu wapendwa,

Nimeweaalika kwa kusanyiko hili la Makardinali (Consistory), siyo tu kwa ajili ya kuwatakatifuza watakatifu watatu, bali pia kuwatangazieni juu ya uamuzi wenye  umuhimu mkubwa kwa maisha ya Kanisa.  Baada ya kutafakari dhamiri yangu mbele ya Mungu tena na tena, nimeona kwa hakika nguvu zangu, kutokana na kuwa na umri  mkubwa, hazitoshi kuweza kutimiza utume wa Upapa kikamilifu. Najua wazi kwamba utume huu, kutokana na umuhimu wa hulka yake ya Kiroho, unapaswa kutekelezwa si tu kwa maneno na matendo, bali pia kwa sala na mateso. Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo, unaokumbwa na  mabadilikko makubwa na kutikiswa na  maswali yenye umuhimu wakina mintarafu maisha ya imani, ili kuongoza mashua ya Petro na kutangaza Injili, nguvu ya akili na mwili ni vya lazima, nguvu ambazo  katika kipindi cha miezi michache iliyopita zimenipungua kiasi cha kugundua kutokuwa na uwezo wa kutekeleza kikamilifu utume niliokabidhiwa. Kwa sababu hiyo, nikijua wazi uzito wa tendo hili, kwa uhuru kamili, natamka kuachia utume wa Askofu wa Roma, Halifa wa Mtume Petro, ambao nilikabidhiwa na Makardinali tarehe 19 April 2005, hivi kwamba kuanzia tarehe 28 Februari 2013, saa 2.00 usiku Kiti cha Roma, Kiti cha Mtume Petro kitakuwa wazi na mkutano wa kumchagua Baba Mtakatifu mpya (conclave) unapaswa kuitishwa na wale walio na mamlaka hayo.

Ndugu wapendwa, ninawashukuru sana kwa upendo wa kazi ambazo mlinisaidia katika utume  wangu na ninaomba radhi kwa mapungufu yangu yote. Na  sasa, tulikabidhiwa Kanisa Takatifu chini ya ulinzi wa Mchungaji Mkuu, Bwana Wetu Yesu Kristo, na tumwombe Mama yake Mtakatifu Maria, ili awasaidie Mababa Kardinali kwa maongezi yake ya kimama katika kumchagua Baba Mtakatifu mpya. Kwa upande wangu, ningependa katika siku zijazo kulihudumia Kanisa Takatifu la Mungu kwa njia ya maisha ya sala.”

Kutoka VATIKANO,  10 FEBRUARI 2013

BENEDICTUS PP XVI

Hii haitakuwa mara ya kwanza kwa Baba Mtakatifu kuachilia madaraka.  Historia inaonesha kuwa Baba Watakatifu kati ya  sita (6) na kumi (10) wamekwishaachia nafasi hiyo. Hawa ni pamoja na  Klementi I (92-201), Pontiano (230-235), Siriakusi, Marsellino (296-304), Martin I (649-655), Benedikto V (964), Benedikto IX (1032-1045) Gregori VI (1045-1046) Celestino V (1294) na Gregori XII (1106-1415).

Friday, January 25, 2013

Siku kuu ya Uongofu wa Mtume Paulo

Sikukuu ya Wongofu wa Mtume Paulo ni sikukuu inayoadhimishwa katika mwaka wa kiliturujia Januari 25, ikinukuu uongofu wake. Mbali na kanisa Katoliki, sikukuu hia pia inaadhimishwa na makanisa mbalimbali ya Mashariki Orthodox, Oriental Orthodox, Anglikana na makanisa ya Kilutheri. Kutokana na kuadhimishwa na makanisa haya mbalimbali, sikukuu hii inakua ni hitimisho la wiki ya maombi ya kuombea Umoja wa Wakristu duniani. Wiki hii ya maombi hufanyika kila mwaka kuanzia Januari 18 mpaka Januari 25


Mtakatifu Paulo alizaliwa kati ya miaka 7-10 BK katika familia ya Kiyahudi ya kabila la Benyamini (Israeli) na madhehebu ya Mafarisayo iliyoishi katika mji wa Tarsus (kwa sasa mji huo uko sehemu ya kusini mashariki ya nchi ya Uturuki).
Jina lake la kwanza (la Kiebrania) lilikuwa Sauli, lakini kadiri ya desturi ya wakati ule alikuwa pia na jina la Kigiriki: Paulos kutoka Kilatini Paulus. Mwenyewe alikuwa na uraia wa Roma kama wananchi wote wa Tarsus. Angali kijana alisomea ualimu wa Sheria (yaani wa Torati) huko Yerusalemu chini ya mwalimu maarufu Gamalieli wa madhehebu ya MafarisayoAkishika dini yake kwa msimamo mkali akawa anapinga Ukristo kwa kuwakamata, kuwatesa na hata kuwaua Wakristo, kama vile Stefano Mfiadini mpaka alipotokewa na Yesu Kristo mfufuka akiwa njiani kwenda Damaski (kwa umuhimu wake katika historia ya wokovu habari hii inasimuliwa mara tatu katika kitabu cha Matendo ya Mitume: 9:1-19; 21:12-18 na 22:5-16). Jibu lake kwa Yesu lilikuwa (Mdo 22:10): "Nifanye nini, Bwana?"

Baada ya Wongofu na baada ya kufanya utume katika mazingira ya Kiarabu, Tarsus na Antiokia alianza kufanya safari za kitume, akienda mbali zaidi na zaidi, akilenga kumhubiri Yesu mahali ambapo bado hajafahamika, hata Hispania.
Ilikuwa kawaida yake kuanzisha Kanisa katika miji mikubwa ili toka huko ujumbe ufike hadi vijijini.
Muda wote wa utume wake Paulo alipambana na dhuluma kutoka kwa Wayahudi wenzake na matatizo mengine kutoka Wakristo wenye msimamo tofauti na wa kwake hasa kuhusu haja ya kufuata masharti ya Agano la Kale ili kupata wokovu.
Hatimaye alikamatwa na wapinzani wake Wayahudi mjini Yerusalemu, lakini askari wakoloni walizuia asiuawe. Baada ya hapo alilazimika kukaa gerezani akisubiri hukumu ya Dola la Roma, kwanza Kaisaria Baharini miaka miwili, halafu akakata rufaa kwa Kaisari akapelekwa Roma, alipofika mwaka 61 akakaa miaka miwili tena kifungo cha nje katika nyumba ya kupanga.

Aliuawa nje ya kuta za Roma kwa kukatwa kichwa wakati wa dhuluma za Nero kati ya mwaka 64 na 67 B.K. Kati ya barua nyingi alizoandikwa kwa makanisa ya Thesalonike, Korintho, Galatia, Roma, Filipi, Kolosai,Efeso, kwa viongozi Wakristo kama Timotheo na Tito, tena kwa Filemoni, katika Agano Jipya zinatunzwa 13. Ukubwa na ubora wa mchango wa Paulo unaeleweka tukizingatia kwamba alifanya kazi na kuandika kabla ya vitabu vya Agano Jipya kupatikana. Ndiye aliyeanza kuliandika akipanua mawazo aliyoyapokea katika Kanisa kwa kuzingatia Agano la Kale na mang’amuzi yake mwenyewe.










Saturday, January 12, 2013

Tafakari ya Sikukuu ya Ubatizo wa Bwana

Sikukuu ya Ubatizo wa Bwana ni sikukuu yetu. Ni sikukuu inayotukumbusha ubatizo wetu. Tunapofanya sherehe hii, swali linalokuja kichwani mara moja ni hili: ubatizo wa Yohane ni ubatizo wa toba, iweje Yesu asiye na dhambi abatizwe? Yesu mwenyewe anajibu swali hili katika Injili ya Matayo. Wakati Yohane anasitasita kumbatiza, Yesu anamwambia:“Kubali sasa hivi; kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote“ (Mt 3: 15).

Yesu anataka “kutimiza haki yote“. Katika kutwaa mwili anatwaa ubinadamu dhaifu, na katika ubatizo wake anatwaa dhambi ya ulimwengu. Anataka “kutimiza haki yote“, ile haki ambayo wazazi wetu wa kwanza wangepaswa kuitimiza; yaani, kuisikiliza sauti ya Mungu na kutimiza mapenzi ya yule aliyewaumba. Utii wa Yesu unaifungua mbingu. Mbingu zilizofungwa kwa dhambi, zinafunguliwa kupitia yule aliyekuwa tayari kutimiza haki ya Mungu. Mbingu zinafunguka, ili Mungu apate kumfunua Yesu kama mwana wake mpendwa. Ni mwana mpendwa kwa sababu yuko tayari kutimiza haki yote ya Mungu. Mbingu zinafunguka ili kwamba sisi kwa kupitia yeye, aliye mlango tufunguliwe mlango wa mbingu kama tutatimiza haki yote. Kuanzia hapo sote tunakuwa wana wa Mungu katika Mwana wa Mungu.



Ubatizo ndiyo mlango wa imani. Imani ndiyo inayotuelekeza kwa Mungu. Wakati wa Kanisa la mwanzo mtu aliulizwa: “Unaomba nini katika Kanisa?“ Naye alipaswa kujibu, “imani“. Imani ndiyo mlango wazi unaotuelekeza kwa Mungu. Imani ndiyo miguu inayotuwezesha kutembea na kuingia kupitia “mbingu zilizofunguka“.

Tuesday, January 8, 2013

Epifania - Siku kuu ya Toleo la Bwana

Kila tarehe 6 Januari,  Kanisa linasheherekea   Siku kuu ya "Toleo la Bwana" inayotambulika kama Epifania. Hii ni Sherehe ambayo Mfalme Masiha anajitambulisha wazi katika Ulimwengu. Injili ya Mathayo 2:1-2 inazungumzia Mamajuzi waliofuata mwongozo wa nyota ili wakamwone Masiha na kumsujudia. Ni kwa njia ya nyota, Mamajusi wanaweza kufika mahali alipokuwa na wakaweza kumsujudia na kumpatia zawadi zao. Kumbe Yesu Kristo Masiha ni nyota inayaangaza na kuongoza maisha yetu mpaka mwisho wa nyakati hadi kufika mbinguni. Katika Siku kuu ya Krismasi tarehe 25 Disemba, Kristo anajitoa katika watu ulimwenguni. Siku kuu ya Toleo la Bwana yaani "Epifania" Mamajusi wanawakilisha watu wote ulimwenguni wanaojitolea kwa Bwana kwa kumwabudu, kumwamini na kumsujudia