Saturday, January 12, 2013

Tafakari ya Sikukuu ya Ubatizo wa Bwana

Sikukuu ya Ubatizo wa Bwana ni sikukuu yetu. Ni sikukuu inayotukumbusha ubatizo wetu. Tunapofanya sherehe hii, swali linalokuja kichwani mara moja ni hili: ubatizo wa Yohane ni ubatizo wa toba, iweje Yesu asiye na dhambi abatizwe? Yesu mwenyewe anajibu swali hili katika Injili ya Matayo. Wakati Yohane anasitasita kumbatiza, Yesu anamwambia:“Kubali sasa hivi; kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote“ (Mt 3: 15).

Yesu anataka “kutimiza haki yote“. Katika kutwaa mwili anatwaa ubinadamu dhaifu, na katika ubatizo wake anatwaa dhambi ya ulimwengu. Anataka “kutimiza haki yote“, ile haki ambayo wazazi wetu wa kwanza wangepaswa kuitimiza; yaani, kuisikiliza sauti ya Mungu na kutimiza mapenzi ya yule aliyewaumba. Utii wa Yesu unaifungua mbingu. Mbingu zilizofungwa kwa dhambi, zinafunguliwa kupitia yule aliyekuwa tayari kutimiza haki ya Mungu. Mbingu zinafunguka, ili Mungu apate kumfunua Yesu kama mwana wake mpendwa. Ni mwana mpendwa kwa sababu yuko tayari kutimiza haki yote ya Mungu. Mbingu zinafunguka ili kwamba sisi kwa kupitia yeye, aliye mlango tufunguliwe mlango wa mbingu kama tutatimiza haki yote. Kuanzia hapo sote tunakuwa wana wa Mungu katika Mwana wa Mungu.



Ubatizo ndiyo mlango wa imani. Imani ndiyo inayotuelekeza kwa Mungu. Wakati wa Kanisa la mwanzo mtu aliulizwa: “Unaomba nini katika Kanisa?“ Naye alipaswa kujibu, “imani“. Imani ndiyo mlango wazi unaotuelekeza kwa Mungu. Imani ndiyo miguu inayotuwezesha kutembea na kuingia kupitia “mbingu zilizofunguka“.

No comments:

Post a Comment