Wednesday, February 13, 2013

KWARESIMA

“Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuomboleza. Rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie  Bwana…” (Yoe 2:12)

Leo Kanisa limeanza kipindi cha Kwaresima. Hizi ni siku arobaini za sala, mafungo, kujinyima, kutubu na kuwasaidia wahitaji. Ni kipindi cha maandalizi ya sikukuu ya Ufufuko wa Yesu. Neno linalotuongoza ni wongofu. Kwaresima ni safari inayomrudisha mkristo kwenye njia ya wongofu: nirudieni mimi! Hivyo ndivyo Bwana anavyotuhimiza. Anataka tumrudie, si kwa matendo ya nje, bali kwa mioyo yetu yote kwa kurarua mioyo na si mavazi.


Mafungo ya Kwaresima si ya kujikatalia kula tu, bali pia kuacha kabisa mawazo, maneno na matendo yanayopunguza mwendo wetu wa safari ya kiroho. Ni kipindi cha ibada ya moyo na cha kutenda matendo ya huruma yanayoonesha mshikamano wa kibinadamu na upendo wa kikristo unaookoa. Kama anavyosema Mt. Petro Krisologo; “Matendo ya huruma na ibada ndiyo mabawa ya mfungo… mfungo bila matendo ya huruma ni sanamu ya njaa, ni muonekano wa nje usio na thamani ya utakatifu. Bila ibada mfungo ni fursa ya ubinafsi… tunapofunga, ndugu zangu, tuweke chakula chetu mikononi mwa maskini” (Petro Krisologo, Omelia VIII, Sul digiuno della Quinquagesima)

Kipindi hiki kinapaswa kuwa kipindi kinachotusaidia kuanza tukio la kinabii, tukio linalosaidia kuyabadili maisha yetu na ya wenzetu. Katika Biblia Musa anafunga siku arobaini usiku na mchana kabla ya kupokea Amri Kumi za Mungu (Rej. Kut 34:28), anafanya hivyo pia Elia kabla hajakutana na Mungu juu yam lima Horebu (1Fal 19:8), hali kadhalika Yesu kabla hajaanza utume wake.

Majivu na maji


Kipindi cha Kwaresima kinaanza siku ya Jumatano ya Majivu. Don Tonino Bello, aliyekuwa Askofu wa Molfetta, Italia anaandika kuwa safari yote ya mkristo ni kuanzia kichwani hadi miguuni. Ni safari inayoelezwa vizuri kwa ishara ya majivu tunayopakwa kichwani na maji anayotumia Yesu kuwaosha mitume wake miguu. Ni safari inayoanzia kwenye toba na kuishia kwenye utumishi. “Toba na utumishi”, anasema Don Tonino Bello, “ni mahubiri makuu ambayo kanisa linayakabidhi kwa majivu na maji, kuliko kwa maneno”. Kwa maneno mengine ndiyo kusema kuwa mahubiri yetu hayawezi kuielezea vizuri zaidi safari ya uongofu kama jinsi ambavyo ishara ya majivu na maji inavyoweza kufanya. Tumrudie Mungu kwa moyo wa toba na katika utumishi tuzidi kuiona ile sura ya Mungu katika mahujaji wote walio katika safari ya maisha. 



No comments:

Post a Comment