Tuesday, February 12, 2013

BENEDIKTO XVI ATANGAZA KUACHILIA MADARAKA YA KULIONGOZA KANISA

Baba Mtakatifu Benedikto XVI ametangaza azma yake ya kuachilia madaraka ya kuliongoza Kanisa Katoliki ifikapo tarehe 28 Februari 2013. Habari hii imepokelewa kwa hisia tofauti na kwa mshtuko mkubwa. Kulingana na taratibu za Kanisa, Baba Mtakatifu anaweza kuachilia madaraka. Sheria ya Kanisa No. 332#2 inaeleza kuwa masharti mawili ya Baba Mtakatifu kuachilia madaraka ya kuliongoza Kanisa, kwanza, ni kufikia uamuzi huo yeye mwenyewe kwa uhuru na kwa hiari yake. 


Pili, ataamke waziwazi juu ya uamuzi wake wa kuachilia madaraka. Baba Mtakatifu anaweza kuachilia madaraka pale anapopoteza uwezo wa kuongoza au inapotokea afya yake ikatetereka na hivi kushindwa kutimiza majukumu yake kikamilifu. Sababu iliyopelekea Baba Mtakatifu Benedikto XVI, ambaye tarehe 16 Aprili atatimiza miaka 85, kuachilia madaraka, kama alivyoeleza mwenyewe ni kutokana na kutetereka kwa afya yake. Akitangaza hatua yake ya kuachilia madaraka aliyoisoma kwa lugha ya kilatini, Baba Mtakatifu Benedikto XVI alisema:


“Ndugu wapendwa,

Nimeweaalika kwa kusanyiko hili la Makardinali (Consistory), siyo tu kwa ajili ya kuwatakatifuza watakatifu watatu, bali pia kuwatangazieni juu ya uamuzi wenye  umuhimu mkubwa kwa maisha ya Kanisa.  Baada ya kutafakari dhamiri yangu mbele ya Mungu tena na tena, nimeona kwa hakika nguvu zangu, kutokana na kuwa na umri  mkubwa, hazitoshi kuweza kutimiza utume wa Upapa kikamilifu. Najua wazi kwamba utume huu, kutokana na umuhimu wa hulka yake ya Kiroho, unapaswa kutekelezwa si tu kwa maneno na matendo, bali pia kwa sala na mateso. Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo, unaokumbwa na  mabadilikko makubwa na kutikiswa na  maswali yenye umuhimu wakina mintarafu maisha ya imani, ili kuongoza mashua ya Petro na kutangaza Injili, nguvu ya akili na mwili ni vya lazima, nguvu ambazo  katika kipindi cha miezi michache iliyopita zimenipungua kiasi cha kugundua kutokuwa na uwezo wa kutekeleza kikamilifu utume niliokabidhiwa. Kwa sababu hiyo, nikijua wazi uzito wa tendo hili, kwa uhuru kamili, natamka kuachia utume wa Askofu wa Roma, Halifa wa Mtume Petro, ambao nilikabidhiwa na Makardinali tarehe 19 April 2005, hivi kwamba kuanzia tarehe 28 Februari 2013, saa 2.00 usiku Kiti cha Roma, Kiti cha Mtume Petro kitakuwa wazi na mkutano wa kumchagua Baba Mtakatifu mpya (conclave) unapaswa kuitishwa na wale walio na mamlaka hayo.

Ndugu wapendwa, ninawashukuru sana kwa upendo wa kazi ambazo mlinisaidia katika utume  wangu na ninaomba radhi kwa mapungufu yangu yote. Na  sasa, tulikabidhiwa Kanisa Takatifu chini ya ulinzi wa Mchungaji Mkuu, Bwana Wetu Yesu Kristo, na tumwombe Mama yake Mtakatifu Maria, ili awasaidie Mababa Kardinali kwa maongezi yake ya kimama katika kumchagua Baba Mtakatifu mpya. Kwa upande wangu, ningependa katika siku zijazo kulihudumia Kanisa Takatifu la Mungu kwa njia ya maisha ya sala.”

Kutoka VATIKANO,  10 FEBRUARI 2013

BENEDICTUS PP XVI

Hii haitakuwa mara ya kwanza kwa Baba Mtakatifu kuachilia madaraka.  Historia inaonesha kuwa Baba Watakatifu kati ya  sita (6) na kumi (10) wamekwishaachia nafasi hiyo. Hawa ni pamoja na  Klementi I (92-201), Pontiano (230-235), Siriakusi, Marsellino (296-304), Martin I (649-655), Benedikto V (964), Benedikto IX (1032-1045) Gregori VI (1045-1046) Celestino V (1294) na Gregori XII (1106-1415).

No comments:

Post a Comment