Sunday, December 30, 2012

MWAKA WA IMANI


Katika waraka wake wa Kitume Porta Fidei (Mlango wa Imani) wa  tarehe  11 Oktoba 2011, Baba Mtakatifu Benedikto XVI alitangaza Mwaka wa Imani ulioanza tarehe 11 Oktoba 2012 na utakaofikia kilele chake tarehe 24 Novemba 2013. Katika hati hiyo, Baba Mtakatifu anawaalika Wakatoliki wote duniani kurudia upya imani yao kwa Baba, kwa Mwana na kwa Roho Mtakatifu na kurudia upya imani yao katika mafundisho ya msingi ya Kanisa. Mwaka wa Imani unaadhimisha pia matukio matatu ya kihistoria:



  • Tukio la kwanza ni kumbukumbu ya miaka 50 tangu  ulipoanza rasmi Mtaguso wa pili wa Vatikano (11 Oktoba 1962).


 Huo uliitishwa na Baba Mtakatifu Yohane XXIII na uliwajumuisha maaskofu wote wa Kanisa Katoliki. Mtaguso ulianza mwaka 1962 na kufungwa mwaka 1965 ukitoa hati 16 za Mtaguso zilizotoa mwongozo wa kichungaji juu ya masuala mbalimbali yanayohusu Kanisa na jamii.  Moja ya malengo ya Mwaka wa Imani ni “kusoma kwa ufasaha” hati za Mtaguso na “zizingatiwe kuwa matini muhimu za kisheria” za mamlakafunzi ya Kanisa (Porta Fidei, 5).


  •  Tukio la pili ni kumbukumbu ya  miaka 20 tangu ilipochapwa rasmi Katekisimu ya Kanisa Katoliki (11 Oktoba 1992).

  Mwaka wa Imani ni fursa ya kuwasaidia Wakatoliki “kuvumbua upya na kujifunza msingi wa mafundisho ya imani  unayopata muhtasari wake ulionyambuliwa na wa kimantiki katika Katekisimu ya Kanisa Katoliki (Porta Fidei, 11).








  •  Tukio la tatu ni Sinodi ya kawaida ya Maaskofu juu ya uinjilishaji Mpya, ambayo  ilifanyika Roma tarehe 7-28 Oktoba 2012.

   Mada ya Sinodi hiyo ilikuwa ni “Uinjilishaji Mpya kwa ajili ya kueneza imani ya kikristo”.  Baba Mtakatifu anapenda Mwaka wa Imani uwasaidie wakristo “kutangaza neno la ukweli ambalo Bwana alituachia” (Porta Fidei, 6) kwa sababu “upendo wa Kristo unatubidisha ... kuinjilisha” (Porta Fidei, 7). Pia “Imani inakuwa pale inapotiwa katika maisha kama uzoefu wa upendo ilipokelewa na pala inaposhirikishwa kwa wengine kama uzoefu wa neema na furaha” (Porta Fidei, 7).




2 comments:

  1. TUMSIFU YESU KRISTU. NAMSHUKURU BABA MTAKATIFU BENEDIKTO XVI KUTANGAZA MWAKA WA IMANI – KUANZIA 11 OKTOBA 2012 NA KUFIKIA KILELE CHAKE 24 NOVEMBA 2013 NA HATA KUTOA BARUA YA KITUME (PORTAL FIDEL) MLANGO WA IMANI. NI UKWELI USIOPINGIKA KUONA KWAMBA WAKATOLIKI WENGI SIKU HIZI TUNAIISHI IMANI YETU JUU JUU TU. KUPITIA MLANGO WA IMANI TUNAALIKWA TUEPUKE KUTOKA IMANI YA MAZOEA NA TUIISHI IMANI YA UKWELI, IMANI YA KINA. PIA KATIKA HII BARUA TUNAHIMIZWA UINJILISHAJI MPYA KWANI MOJA YA MATATIZO MAKUBWA LEO KATIKA KANISA LETU NI UKOSEKANAJI WA KATEKESI KWA WAUMINI WAKE.

    SASA NAOMBA NIFAFANULIWE, KATIKA UINJILISHAJI MPYA NA WA KINA, SISI KAMA WAKATOLIKI TUNATUMAINI AU TUNATEGEMEA MABADILIKO GANI IWAPO TUNAENDELEA NA MAFUNDISHO YA MASWALI NA MAJIBU KWA KUTUMIA KATEKISIMU ZETU KATIKA KUWAPATIA WENZETU MAFUNDISHO KANISANI? SINA UHAKIKA KAMA MTINDO HUU WA UWAANDAAJI WA WAKATUKUMENI, MAFUNDISHO YA KOMUNYO YA KWANZA, KIPAIMARA N.K. MAKANISA YOTE TUNATUMIA MASWALI NA MAJIBU YALIYOANDALIWA KATIKA KATEKESIMU ZETU NA MTAHINIWA AKIULIZWA SWALI NA AKAJIBU SAHIHI, HATA KAMA ALIKARIRI TU JIBU NA HAELEWI MAANA YAKE BASI ANABATIZWA, ANAPATA KOMUNYO NA ANAPATA KIPAIMARA. LAKINI KWENYE PAROKIA AMBAZO MIMI NIMEISHI NIMEYAONA HAYA. TUTAFAULU KATIKA UINJILISHAJI UPYA KWA NAMNA HII?

    ReplyDelete
  2. Tumsifu Yesu Kristu,
    Mafundisho ya Kanisa kupitia Katekisimu na Biblia bado yanabaki kama misingi ya ufundishaji na ukuzaji wa Imani Katoliki. Njia hii ya kukuza na kulinda Imani ya Kristu haitoweza badilika kamwe.

    Uinjilishaji mpya si jitihada mpya bali ni jitihada zilizohimizwa hata na Mwenye Heri Papa Yohane wa Pili toka miaka ya themanini.
    Ni muhimu kukumbuka kuwa Kanisa linajengwa na waumini wote na si mkusanyiko wa Askofu, Padre na Shemani. Mwenye heri Papa Yohane wa pili pamoja na Baba Mtakatifu Benedikto wanasisitiza kazi ya Uinjilishaji Mpya ni ya waumini wote wa ngazi zote. Ni kila muumini kupitia taaluma na karama alizopewa na Roho Mtakatifu analo jukumu la kumshuhudia Kristu kwa wote. Mkatoliki yabidi afanye uinjilishaji katika Jumuiya ndogo ndogo, katika vyama mbalimbali vya Mitume, katika vikundi vya vijana, katika usomaji wa Biblia akizingatia mafundisho ya Kanisa.

    Kanisa pia laipa nafasi kubwa teknolojia ya Internet katika uinjilishaji. Vijana wengi wanapatikana katika tovuti za Facebook, Blogs, Twitter, LinkedIn, Youtube. Basi inakua ni vyema kwa kupitia vyanzo hivi vya habari Kristu aweze kuhubiriwa. Mfano huu auonyesha Baba Mtakatifu ambaye hutumia vyombo hivi mara kwa mara katika malengo ya kuwafikia wakristu kokote pale waliko

    ReplyDelete