Wednesday, February 13, 2013

KWARESIMA

“Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuomboleza. Rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie  Bwana…” (Yoe 2:12)

Leo Kanisa limeanza kipindi cha Kwaresima. Hizi ni siku arobaini za sala, mafungo, kujinyima, kutubu na kuwasaidia wahitaji. Ni kipindi cha maandalizi ya sikukuu ya Ufufuko wa Yesu. Neno linalotuongoza ni wongofu. Kwaresima ni safari inayomrudisha mkristo kwenye njia ya wongofu: nirudieni mimi! Hivyo ndivyo Bwana anavyotuhimiza. Anataka tumrudie, si kwa matendo ya nje, bali kwa mioyo yetu yote kwa kurarua mioyo na si mavazi.


Mafungo ya Kwaresima si ya kujikatalia kula tu, bali pia kuacha kabisa mawazo, maneno na matendo yanayopunguza mwendo wetu wa safari ya kiroho. Ni kipindi cha ibada ya moyo na cha kutenda matendo ya huruma yanayoonesha mshikamano wa kibinadamu na upendo wa kikristo unaookoa. Kama anavyosema Mt. Petro Krisologo; “Matendo ya huruma na ibada ndiyo mabawa ya mfungo… mfungo bila matendo ya huruma ni sanamu ya njaa, ni muonekano wa nje usio na thamani ya utakatifu. Bila ibada mfungo ni fursa ya ubinafsi… tunapofunga, ndugu zangu, tuweke chakula chetu mikononi mwa maskini” (Petro Krisologo, Omelia VIII, Sul digiuno della Quinquagesima)

Kipindi hiki kinapaswa kuwa kipindi kinachotusaidia kuanza tukio la kinabii, tukio linalosaidia kuyabadili maisha yetu na ya wenzetu. Katika Biblia Musa anafunga siku arobaini usiku na mchana kabla ya kupokea Amri Kumi za Mungu (Rej. Kut 34:28), anafanya hivyo pia Elia kabla hajakutana na Mungu juu yam lima Horebu (1Fal 19:8), hali kadhalika Yesu kabla hajaanza utume wake.

Majivu na maji


Kipindi cha Kwaresima kinaanza siku ya Jumatano ya Majivu. Don Tonino Bello, aliyekuwa Askofu wa Molfetta, Italia anaandika kuwa safari yote ya mkristo ni kuanzia kichwani hadi miguuni. Ni safari inayoelezwa vizuri kwa ishara ya majivu tunayopakwa kichwani na maji anayotumia Yesu kuwaosha mitume wake miguu. Ni safari inayoanzia kwenye toba na kuishia kwenye utumishi. “Toba na utumishi”, anasema Don Tonino Bello, “ni mahubiri makuu ambayo kanisa linayakabidhi kwa majivu na maji, kuliko kwa maneno”. Kwa maneno mengine ndiyo kusema kuwa mahubiri yetu hayawezi kuielezea vizuri zaidi safari ya uongofu kama jinsi ambavyo ishara ya majivu na maji inavyoweza kufanya. Tumrudie Mungu kwa moyo wa toba na katika utumishi tuzidi kuiona ile sura ya Mungu katika mahujaji wote walio katika safari ya maisha. 



Tuesday, February 12, 2013

BENEDIKTO XVI ATANGAZA KUACHILIA MADARAKA YA KULIONGOZA KANISA

Baba Mtakatifu Benedikto XVI ametangaza azma yake ya kuachilia madaraka ya kuliongoza Kanisa Katoliki ifikapo tarehe 28 Februari 2013. Habari hii imepokelewa kwa hisia tofauti na kwa mshtuko mkubwa. Kulingana na taratibu za Kanisa, Baba Mtakatifu anaweza kuachilia madaraka. Sheria ya Kanisa No. 332#2 inaeleza kuwa masharti mawili ya Baba Mtakatifu kuachilia madaraka ya kuliongoza Kanisa, kwanza, ni kufikia uamuzi huo yeye mwenyewe kwa uhuru na kwa hiari yake. 


Pili, ataamke waziwazi juu ya uamuzi wake wa kuachilia madaraka. Baba Mtakatifu anaweza kuachilia madaraka pale anapopoteza uwezo wa kuongoza au inapotokea afya yake ikatetereka na hivi kushindwa kutimiza majukumu yake kikamilifu. Sababu iliyopelekea Baba Mtakatifu Benedikto XVI, ambaye tarehe 16 Aprili atatimiza miaka 85, kuachilia madaraka, kama alivyoeleza mwenyewe ni kutokana na kutetereka kwa afya yake. Akitangaza hatua yake ya kuachilia madaraka aliyoisoma kwa lugha ya kilatini, Baba Mtakatifu Benedikto XVI alisema:


“Ndugu wapendwa,

Nimeweaalika kwa kusanyiko hili la Makardinali (Consistory), siyo tu kwa ajili ya kuwatakatifuza watakatifu watatu, bali pia kuwatangazieni juu ya uamuzi wenye  umuhimu mkubwa kwa maisha ya Kanisa.  Baada ya kutafakari dhamiri yangu mbele ya Mungu tena na tena, nimeona kwa hakika nguvu zangu, kutokana na kuwa na umri  mkubwa, hazitoshi kuweza kutimiza utume wa Upapa kikamilifu. Najua wazi kwamba utume huu, kutokana na umuhimu wa hulka yake ya Kiroho, unapaswa kutekelezwa si tu kwa maneno na matendo, bali pia kwa sala na mateso. Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo, unaokumbwa na  mabadilikko makubwa na kutikiswa na  maswali yenye umuhimu wakina mintarafu maisha ya imani, ili kuongoza mashua ya Petro na kutangaza Injili, nguvu ya akili na mwili ni vya lazima, nguvu ambazo  katika kipindi cha miezi michache iliyopita zimenipungua kiasi cha kugundua kutokuwa na uwezo wa kutekeleza kikamilifu utume niliokabidhiwa. Kwa sababu hiyo, nikijua wazi uzito wa tendo hili, kwa uhuru kamili, natamka kuachia utume wa Askofu wa Roma, Halifa wa Mtume Petro, ambao nilikabidhiwa na Makardinali tarehe 19 April 2005, hivi kwamba kuanzia tarehe 28 Februari 2013, saa 2.00 usiku Kiti cha Roma, Kiti cha Mtume Petro kitakuwa wazi na mkutano wa kumchagua Baba Mtakatifu mpya (conclave) unapaswa kuitishwa na wale walio na mamlaka hayo.

Ndugu wapendwa, ninawashukuru sana kwa upendo wa kazi ambazo mlinisaidia katika utume  wangu na ninaomba radhi kwa mapungufu yangu yote. Na  sasa, tulikabidhiwa Kanisa Takatifu chini ya ulinzi wa Mchungaji Mkuu, Bwana Wetu Yesu Kristo, na tumwombe Mama yake Mtakatifu Maria, ili awasaidie Mababa Kardinali kwa maongezi yake ya kimama katika kumchagua Baba Mtakatifu mpya. Kwa upande wangu, ningependa katika siku zijazo kulihudumia Kanisa Takatifu la Mungu kwa njia ya maisha ya sala.”

Kutoka VATIKANO,  10 FEBRUARI 2013

BENEDICTUS PP XVI

Hii haitakuwa mara ya kwanza kwa Baba Mtakatifu kuachilia madaraka.  Historia inaonesha kuwa Baba Watakatifu kati ya  sita (6) na kumi (10) wamekwishaachia nafasi hiyo. Hawa ni pamoja na  Klementi I (92-201), Pontiano (230-235), Siriakusi, Marsellino (296-304), Martin I (649-655), Benedikto V (964), Benedikto IX (1032-1045) Gregori VI (1045-1046) Celestino V (1294) na Gregori XII (1106-1415).